Baba Ajibu Dhiki ya Hezekia
19 1Mfalme Hezekia aliposikia haya, alirarua mavazi yake, akavaa nguo za magunia, akaingia katika nyumba ya Baba yetu. 2Akamtuma Eliakimu msimamizi wa nyumba ya mfalme, na Shebna mwandishi, na wazee wa makuhani, wote wamevaa nguo za magunia, kwa nabii Isaya mwana wa Amozi. 3Wakamwambia, "Hezekia asema: Leo ni siku ya dhiki, na ya karipio, na ya aibu; watoto wamefikia wakati wa kuzaliwa, lakini hakuna nguvu za kuwazaa. 4Huenda Baba yako atayasikia maneno yote ya jemadari wa jeshi, ambaye bwana wake mfalme wa Ashuru amemtuma kumdhihaki Baba aliye hai, naye atayahukumu maneno aliyoyasikia. Basi omba kwa ajili ya mabaki yaliyosalia."
5Watumishi wa mfalme Hezekia walipofika kwa Isaya,
6Isaya akawaambia, "Mwambieni bwana wenu Baba yetu asema hivi: Usiogope maneno uliyoyasikia, ambayo watumishi wa mfalme wa Ashuru wamenitukana kwayo. 7Tazama, nitatia roho ndani yake: atasikia habari, atarudi katika nchi yake mwenyewe, nami nitamfanya aanguke kwa upanga huko katika nchi yake."
8Yule jemadari wa jeshi aliposikia ya kwamba mfalme wa Ashuru ameondoka Lakishi, akarudi, akamkuta akipigana na Libna. 9Basi mfalme akasikia habari za Tirhaka mfalme wa Kushi, kusema, "Tazama, ametoka kupigana nawe." Naye akatuma tena wajumbe kwa Hezekia, kusema: 10"Mwambieni Hezekia mfalme wa Yuda: Mungu wako, unayemtumaini, asikudanganye kwa kusema, Yerusalemu hautatiwa katika mkono wa mfalme wa Ashuru. 11Tazama, umesikia wafalme wa Ashuru walivyozitenda nchi zote, kwa kuziangamiza kabisa. Nawe je, utaokolewa? 12Je, miungu ya mataifa waliyoyaangamiza baba zangu iliwaokoa—Gozani, na Harani, na Resefu, na wana wa Edeni waliokuwa Telasari? 13Yuko wapi mfalme wa Hamathi, na mfalme wa Arpadi, na mfalme wa mji wa Sefarvaimu, na wa Hena, na wa Iva?"
Hezekia Aitandaza Mbele za Baba
14Hezekia akaipokea barua mkononi mwa wajumbe, akaisoma. Kisha akapanda kwenda nyumba ya Baba yetu, akaitandaza mbele zake. 15Hezekia akaomba mbele za Baba yetu, akasema: "Ee Mungu wa Israeli, uketiye juu ya makerubi, wewe ndiwe Mungu peke yako, juu ya falme zote za dunia; wewe ndiwe uliyeziumba mbingu na nchi. 16Tega sikio lako, Baba yetu, ukasikie; fumbua macho yako, ukatazame. Yasikie maneno ya Senakeribu aliyoyapeleka kumdhihaki Baba aliye hai. 17Ni kweli, Baba yetu, wafalme wa Ashuru waliyaangamiza mataifa na nchi zao, 18na kuitupa miungu yao motoni; kwa maana haikuwa miungu, bali kazi ya mikono ya wanadamu, miti na mawe. Kwa hiyo wakaiharibu. 19Basi sasa, Baba yetu, utuokoe na mkono wake, ili falme zote za dunia zipate kujua ya kuwa wewe ndiwe Mungu peke yako."
Baba Adhili Kiburi cha Senakeribu
20Kisha Isaya mwana wa Amozi akatuma kwa Hezekia, kusema: "Baba yetu, Mungu wa Israeli, asema hivi: Nimeyasikia maombi uliyoyaomba kwangu kwa habari ya Senakeribu mfalme wa Ashuru. 21Hili ndilo neno Baba yetu alilolinena juu yake: Bikira, binti Sayuni, amekudharau na kukudhihaki; binti Yerusalemu ametikisa kichwa chake nyuma yako. 22Ni nani uliyemshutumu na kumkufuru? Ni juu ya nani ulioipaza sauti yako na kuyainua macho yako kwa kiburi? Ni juu ya yeye Mtakatifu wa Israeli! 23Kwa wajumbe wako umemdhihaki Baba Mwenye Enzi, nawe umesema: Kwa wingi wa magari yangu ya vita nimepanda vilele vya milima, mahali pa mbali sana pa Lebanoni. Nimeikata mierezi yake mirefu, misunobari yake iliyo bora. Nimefika kwenye kilele chake cha mbali sana, msitu wake ulio mnene. 24Nimechimba visima na kunywa maji ya kigeni; kwa nyayo za miguu yangu nimekausha vijito vyote vya Misri. 25Je, hukusikia? Zamani sana mimi nilifanya jambo hili; tangu siku za kale nilikusudia hilo. Sasa nimelitimiza, kwamba wewe uifanye miji yenye maboma kuwa magofu ya mavumbi. 26Wenyeji wake, walioondolewa nguvu, walifadhaika na kuaibika. Walikuwa kama majani ya kondeni, kama machipukizi mabichi laini, kama nyasi zimeazo juu ya nyumba, zilizoungua kabla hazijakua. 27Lakini mimi ninajua kuketi kwako, na kutoka kwako na kuingia kwako, na jinsi unavyonighadhibikia. 28Kwa sababu ya kunighadhibikia kwako, na kiburi chako kilichofika masikioni mwangu, nitatia ndoana yangu puani mwako na hatamu yangu midomoni mwako, nami nitakurudisha kwa njia ile uliyoijia.
29Nayo hii ndiyo ishara yako, Hezekia: mwaka huu kuleni kiotacho chenyewe, na mwaka wa pili kile kimeacho katika hicho; lakini mwaka wa tatu pandeni, mkavune, mpande mashamba ya mizabibu, mkale matunda yake. 30Na mabaki ya nyumba ya Yuda yaliyosalia yatatia mizizi tena chini, na kuzaa matunda juu. 31Kwa maana kutoka Yerusalemu watatoka mabaki, na kutoka mlima Sayuni kundi la watu waliookoka. Wivu wa Baba wa majeshi ya mbinguni ndio utakaotimiza jambo hili.
32"Basi hivi ndivyo Baba yetu asemavyo kwa habari ya mfalme wa Ashuru: Hataingia katika mji huu, wala hatapiga mshale hapa, wala hataukabili kwa ngao, wala hatafanya boma la kuuhusuru. 33Kwa njia ile aliyoijia atarudi; wala hataingia katika mji huu, asema Baba yetu. 34Kwa maana nitaulinda mji huu ili niuokoe, kwa ajili yangu mwenyewe, na kwa ajili ya Daudi mtumishi wangu."
35Ikawa usiku ule malaika wa Baba yetu akatoka, akawapiga watu mia moja na themanini na tano elfu katika kambi ya Waashuru. Na watu walipoamka asubuhi na mapema—kumbe, hao wote walikuwa maiti. 36Basi Senakeribu mfalme wa Ashuru akaondoka, akaenda zake, akarudi, akakaa Ninawi. 37Ikawa alipokuwa akiabudu katika nyumba ya Nisroki mungu wake, Adrameleki na Shareseri wanawe wakampiga kwa upanga, wakakimbilia nchi ya Ararati. Naye Esarhadoni mwanawe akatawala mahali pake.