Amazia Anatawala Yuda
14 1Katika mwaka wa pili wa Yoashi mwana wa Yehoahazi, mfalme wa Israeli, Amazia mwana wa Yoashi alianza kutawala Yuda. 2Alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala, naye akatawala miaka ishirini na tisa huko Yerusalemu. Jina la mama yake aliitwa Yehoadani wa Yerusalemu. 3Akafanya yaliyo mema machoni pa Baba yetu—lakini si kama Daudi baba yake; akafanya yote aliyoyafanya Yoashi baba yake. 4Ila mahali pa juu hapakuondolewa; watu wakaendelea kutoa dhabihu na kufukiza uvumba huko. 5Ufalme ulipokwisha kuimarika mkononi mwake, akawaua watumishi wake waliokuwa wamemuua mfalme, baba yake.
6Lakini hakuwaua watoto wa hao wauaji, kama ilivyoandikwa katika Kitabu cha Torati ya Musa, ambapo Baba yetu aliamuru, "Baba wasife kwa ajili ya watoto wao, wala watoto kwa ajili ya baba zao; kila mtu atakufa kwa dhambi yake mwenyewe."
7Akawaua Waedomu elfu kumi katika Bonde la Chumvi, akauteka Sela kwa vita, akauita jina lake Yoktheeli, jina lake hata leo.
8Ndipo Amazia akatuma wajumbe kwa Yehoashi mwana wa Yehoahazi, mwana wa Yehu, mfalme wa Israeli, akisema: "Njoo, na tuonane uso kwa uso."
9Lakini Yehoashi mfalme wa Israeli akampelekea jibu Amazia mfalme wa Yuda, akisema: "Mbaruti wa Lebanoni ulituma ujumbe kwa mwerezi wa Lebanoni, ukisema, 'Mpe binti yako mwanangu awe mke wake.' Kisha mnyama wa mwituni wa Lebanoni akapita, akaukanyaga ule mbaruti. 10Umempiga Edomu, na moyo wako umejaa kiburi. Jivune kwa hilo, lakini ukae nyumbani. Kwa nini kutafuta mabaya, uanguke, wewe na Yuda pamoja nawe?"
11Lakini Amazia hakukubali kusikia, hivyo Yehoashi mfalme wa Israeli akakwea, naye pamoja na Amazia mfalme wa Yuda wakaonana uso kwa uso huko Beth-shemeshi katika Yuda. 12Yuda akashindwa mbele ya Israeli, na kila mtu akakimbilia nyumbani kwake. 13Yehoashi mfalme wa Israeli akamteka Amazia mfalme wa Yuda, mwana wa Yehoashi mwana wa Ahazia, huko Beth-shemeshi, akaja Yerusalemu, akabomoa ukuta wake kiasi cha dhiraa mia nne, tangu Lango la Efraimu hata Lango la Pembeni. 14Akachukua dhahabu yote, na fedha, na vyombo vyote vilivyokuwa katika nyumba ya Baba yetu na katika hazina za mfalme, pamoja na mateka, akarudi Samaria.
15Basi mambo yaliyosalia ya Yehoashi, aliyoyafanya, na uweza wake, na jinsi alivyopigana na Amazia mfalme wa Yuda, je! hayakuandikwa katika Kitabu cha Tarehe za Wafalme wa Israeli? 16Yehoashi akalala na baba zake, akazikwa Samaria pamoja na wafalme wa Israeli; na Yeroboamu mwanawe akatawala mahali pake.
17Amazia mwana wa Yoashi, mfalme wa Yuda, akaishi miaka kumi na mitano baada ya kufa kwake Yehoashi mwana wa Yehoahazi, mfalme wa Israeli. 18Na mambo yaliyosalia ya Amazia—je! hayakuandikwa katika Kitabu cha Tarehe za Wafalme wa Yuda? 19Wakafanya shauri baya juu yake huko Yerusalemu; naye akakimbilia Lakishi, lakini wakatuma watu wamfuate mpaka Lakishi, wakamuulia huko. 20Wakamchukua juu ya farasi; akazikwa Yerusalemu pamoja na baba zake, katika Mji wa Daudi.
21Nao watu wote wa Yuda wakamtwaa Azaria, mwenye umri wa miaka kumi na sita, wakamfanya mfalme mahali pa baba yake Amazia. 22Yeye ndiye aliyeujenga tena Elathi na kuurudisha kwa Yuda, baada ya mfalme kulala na baba zake.
Huruma ya Baba juu ya Israeli
23Katika mwaka wa kumi na tano wa Amazia mwana wa Yoashi mfalme wa Yuda, Yeroboamu mwana wa Yoashi mfalme wa Israeli alianza kutawala huko Samaria, akatawala miaka arobaini na mmoja. 24Akafanya yaliyo mabaya machoni pa Baba yetu, wala hakuziacha dhambi zote za Yeroboamu mwana wa Nebati, aliyeifanya Israeli kutenda dhambi. 25Yeye ndiye aliyeurudisha mpaka wa Israeli, tangu Lebo-hamathi hata Bahari ya Araba, kama vile Baba yetu, Mungu wa Israeli, alivyonena kwa kinywa cha mtumishi wake Yona mwana wa Amitai, nabii wa Gath-heferi. 26Kwa maana Baba yetu aliona ya kuwa mateso ya Israeli yalikuwa machungu mno, wala hakuna aliyesalia, mtumwa wala huru, wala hakuna wa kumsaidia Israeli. 27Lakini Baba yetu hakusema ya kwamba atalifuta jina la Israeli chini ya mbingu, hivyo akawaokoa kwa mkono wa Yeroboamu mwana wa Yoashi. 28Basi mambo yaliyosalia ya Yeroboamu, na yote aliyoyafanya, na uweza wake, na jinsi alivyopigana, na jinsi alivyourudisha Dameski na Hamathi kwa Yuda katika Israeli, je! hayakuandikwa katika Kitabu cha Tarehe za Wafalme wa Israeli? 29Yeroboamu akalala na baba zake, wafalme wa Israeli; na Zekaria mwanawe akatawala mahali pake.