Senakeribu Avamia na Hezekia Ajiandaa
32 1Baada ya mambo haya na matendo haya ya uaminifu, Senakeribu, mfalme wa Ashuru, akaivamia Yuda, akayazingira miji yake yenye ngome, akikusudia kuyabomoa ayatwae kwa ajili yake mwenyewe. 2Hezekia alipoona kwamba Senakeribu amekuja, akiwa amenuia kupigana vita dhidi ya Yerusalemu, 3akafanya shauri na maofisa wake na mashujaa wake kuhusu kuzuia chemchemi zilizokuwa nje ya mji, nao wakamsaidia. 4Watu wengi wakakusanyika, wakazizuia chemchemi zote na kijito kilichopita katikati ya nchi, wakisema, "Kwa nini wafalme wa Ashuru waje na kupata maji tele?"
5Akajitahidi sana kuujenga upya ukuta wote uliobomoka, akajenga minara juu yake, akajenga ukuta mwingine nje, akaimarisha Milo ya mji wa Daudi, na akatengeneza silaha tele na ngao. a a v5 Milo ilikuwa mfumo wa udongo uliojazwa katika matuta na kuta za kuzuia zilizojengwa katika kilima cha Mji wa Daudi. 6Akaweka majemadari wa vita juu ya watu, akawakusanya kwenye uwanja wa lango la mji, akawatia moyo: 7"Kuweni hodari na mashujaa. Msiogope wala msifadhaike kwa sababu ya mfalme wa Ashuru na jeshi lake lote, kwa maana walio pamoja nasi ni wengi kuliko walio pamoja naye. 8Pamoja naye kuna mkono wa mwili tu; lakini pamoja nasi yuko Baba yetu, kutusaidia na kupigana vita vyetu." Watu wakayategemea maneno ya Hezekia mfalme wa Yuda.
Senakeribu Amdhihaki Baba yetu
9Baada ya haya, alipokuwa akiuzingira Lakishi pamoja na majeshi yake yote, Senakeribu mfalme wa Ashuru akawatuma watumishi wake Yerusalemu, kwa Hezekia mfalme wa Yuda na kwa Yuda wote waliokuwa huko, akisema: 10"Hivi ndivyo asemavyo Senakeribu mfalme wa Ashuru: Mnategemea nini, hata mkakaa katika kuzingirwa ndani ya Yerusalemu? 11Je, Hezekia hawadanganyi, akiwaacha mfe kwa njaa na kiu, asemapo, 'BWANA Mungu wetu atatuokoa kutoka mkononi mwa mfalme wa Ashuru'? 12Je, si Hezekia yeye yeye aliyeziondoa mahali pake pa juu na madhabahu zake, akiwaambia Yuda na Yerusalemu kuabudu mbele ya madhabahu moja na kufukiza sadaka hapo? 13Je, hamjui nililowafanya mimi na baba zangu kwa watu wote wa nchi nyingine? Je, miungu ya mataifa yao iliweza kuziokoa nchi zao kutoka mkononi mwangu? 14Ni mungu yupi wa mataifa ambayo baba zangu waliyaangamiza kabisa aliyeweza kuwaokoa watu wake kutoka mkononi mwangu? Basi, Mungu wenu atawezaje kuwaokoa ninyi kutoka mkononi mwangu? 15Basi Hezekia asiwadanganye wala asiwapotoshe hivi, wala msimwamini: kwa maana hakuna mungu wa taifa lolote wala ufalme wowote aliyeweza kuwaokoa watu wake kutoka mkononi mwangu au mkononi mwa baba zangu—sembuse Mungu wenu atawaokoa ninyi kutoka mkononi mwangu!"
16Nao watumishi wake wakaendelea kusema zaidi dhidi ya Baba yetu na dhidi ya mtumishi wake Hezekia. 17Pia Senakeribu akaandika barua za kumtukana Baba yetu, Mungu wa Israeli, akinena dhidi yake: "Miungu ya mataifa haikuwaokoa watu wao kutoka mkononi mwangu; kadhalika Mungu wa Hezekia hatawaokoa watu wake kutoka mkononi mwangu." 18Wakapiga kelele kwa sauti kubwa kwa lugha ya Kiyahudi kwa watu wa Yerusalemu waliokuwa juu ya ukuta, ili kuwatia hofu na kuwaogofya, wapate kuutwaa mji. 19Wakanena juu ya Mungu wa Yerusalemu kama juu ya miungu ya watu wa dunia, kazi ya mikono ya wanadamu.
20Ndipo Mfalme Hezekia na nabii Isaya mwana wa Amozi wakaomba kuhusu jambo hili, wakilia kwa mbingu. 21Basi Baba yetu akamtuma malaika aliyemuua kila shujaa hodari, jemadari, na ofisa katika kambi ya mfalme wa Ashuru. Senakeribu akarudi nyumbani kwa aibu, na alipoingia ndani ya nyumba ya mungu wake, baadhi ya wanawe mwenyewe wakamuua humo kwa upanga. 22Hivyo Baba yetu akamwokoa Hezekia na watu wa Yerusalemu kutoka mkononi mwa Senakeribu mfalme wa Ashuru na mkononi mwa wote wengine, akawatunza pande zote. 23Wengi wakaleta zawadi kwa Baba yetu huko Yerusalemu, na hazina kwa Hezekia mfalme wa Yuda; tangu hapo mataifa yote yakamheshimu Hezekia sana.
Ugonjwa, Kiburi, na Fanaka ya Hezekia
24Siku hizo Hezekia akaugua hata karibu ya kufa; akamwomba Baba yetu, naye akamjibu, akampa ishara. 25Lakini Hezekia hakulipa kadiri ya wema aliotendewa; moyo wake ukajaa kiburi, kwa hiyo hasira ikaja juu yake na juu ya Yuda na Yerusalemu. 26Hezekia akajinyenyekeza kwa sababu ya kiburi cha moyo wake, yeye na watu wa Yerusalemu, kwa hiyo ghadhabu ya Baba yetu haikuwafikia katika siku za Hezekia.
27Hezekia alikuwa na utajiri mwingi na heshima. Akajenga ghala za fedha, dhahabu, vito vya thamani, manukato, ngao, na vitu vingine vya thamani, 28ghala za mavuno ya nafaka, divai mpya, na mafuta; mazizi ya kila aina ya wanyama; na vibanda vya makundi ya kondoo. 29Akajijengea miji, akapata makundi makubwa ya kondoo na ng'ombe, kwa maana Baba yetu alimpa utajiri mwingi sana. 30Hezekia akauzuia mfereji wa juu wa maji ya Gihoni, akayaelekeza maji chini upande wa magharibi wa mji wa Daudi. Akafanikiwa katika yote aliyoyafanya. 31Wakuu wa Babeli walipomtuma wajumbe kumuuliza kuhusu ishara iliyotokea katika nchi, Baba yetu akamwacha peke yake, ili kumjaribu na kujua yote yaliyokuwa moyoni mwake.
32Matendo ya Hezekia yaliyosalia na matendo yake ya uaminifu yameandikwa katika njozi ya nabii Isaya, mwana wa Amozi, katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na Israeli. 33Hezekia akalala na baba zake, akazikwa katika makaburi ya juu ya wana wa Daudi. Yuda wote na wakazi wa Yerusalemu wakamheshimu wakati wa kufa kwake. Mwanawe Manase akatawala mahali pake.