Sauli na Wanawe Waanguka Vitani
31 1Wafilisti wakapigana na Israeli; watu wa Israeli wakawakimbia, wakaanguka wamekufa juu ya mlima Gilboa. 2Wafilisti wakawafikia Sauli na wanawe, nao Wafilisti wakawaua Yonathani, na Abinadabu, na Malkishua, wana wa Sauli. 3Vita vikamwelemea Sauli vikali. Wapiga upinde wakamkuta, naye akajeruhiwa vibaya nao. 4Sauli akamwambia mbeba silaha wake, "Futa upanga wako, unichome, wasije watu hawa wasiotahiriwa wakanichoma na kunidhihaki." Lakini mbeba silaha wake akakataa, kwa maana aliogopa sana. Basi Sauli akautwaa upanga wake mwenyewe, akauangukia. 5Mbeba silaha wake alipoona ya kuwa Sauli amekufa, naye pia akauangukia upanga wake, akafa pamoja naye. 6Hivyo Sauli akafa siku hiyo, yeye na wanawe watatu, na mbeba silaha wake, na watu wake wote pamoja.
7Watu wa Israeli waliokuwa ng'ambo ya bonde na ng'ambo ya Yordani walipoona ya kuwa jeshi la Israeli limekimbia, na ya kuwa Sauli na wanawe wamekufa, wakaiacha miji yao, wakakimbia. Wafilisti wakaja, wakakaa ndani yake. 8Siku ya pili yake, Wafilisti wakaja kuwavua nguo waliokufa, wakamkuta Sauli na wanawe watatu wameanguka juu ya mlima Gilboa. 9Wakamkata kichwa, wakamvua silaha zake, wakatuma wajumbe kupita nchi ya Wafilisti wapeleke habari katika mahekalu ya sanamu zao na kati ya watu. 10Wakaziweka silaha zake katika hekalu la Ashtorethi, wakaukaza mwili wake katika ukuta wa Beth-shani. a a v10 Ashtorethi alikuwa mungu wa kike wa Wakanaani; kuziweka silaha za Sauli katika hekalu lake ilikuwa ni namna ya Wafilisti kuipatia miungu yao sifa ya ushindi.
11Wenyeji wa Yabeshi-gileadi waliposikia hayo Wafilisti waliyomtenda Sauli, 12watu wao wote hodari wa vita wakaenda usiku kucha, wakautwaa mwili wa Sauli na miili ya wanawe kutoka ukuta wa Beth-shani, wakaileta Yabeshi, wakaiteketeza kwa moto huko. 13Wakaitwaa mifupa yao, wakaizika chini ya mkwaju huko Yabeshi, wakafunga siku saba.