Daudi Akimbilia Kwa Wafilisti
27 1Daudi akawaza moyoni, "Siku moja nitaangamizwa kwa mkono wa Sauli. Hakuna lililo bora kwangu kuliko kukimbilia mara moja katika nchi ya Wafilisti. Hapo Sauli atakata tamaa ya kunitafuta popote ndani ya mipaka ya Israeli, nami nitaokoka mkononi mwake." 2Daudi akaondoka, akavuka, yeye na wale watu 600 waliokuwa pamoja naye, wakaenda kwa Akishi mwana wa Maoki, mfalme wa Gathi. 3Daudi akakaa na Akishi huko Gathi, yeye na watu wake, kila mmoja na nyumba yake—Daudi na wake zake wawili, Ahinoamu wa Yezreeli na Abigaili wa Karmeli, mjane wa Nabali. 4Sauli alipoambiwa kwamba Daudi amekimbilia Gathi, hakumtafuta tena.
5Daudi akamwambia Akishi, "Kama nimepata kibali machoni pako, nipe mahali katika mojawapo ya miji ya mashambani nikae huko. Kwa nini mtumishi wako akae pamoja nawe katika mji wa kifalme?" 6Siku ile Akishi akampa Siklagi; kwa hiyo Siklagi umekuwa mali ya wafalme wa Yuda hata leo. 7Muda ambao Daudi aliishi katika nchi ya Wafilisti ulikuwa mwaka mmoja na miezi minne.
8Daudi na watu wake wakapanda, wakawavamia Wageshuri, Wagirzi, na Waamaleki, kwa maana hao walikuwa wenyeji wa nchi ile tangu zamani za kale, kuelekea Shuri hata nchi ya Misri. 9Kila mara Daudi alipoishambulia nchi, hakumwacha hai mwanamume wala mwanamke, akachukua kondoo, ng'ombe, punda, ngamia, na mavazi, kisha akarudi kwa Akishi.
10Akishi alikuwa akiuliza, "Mmevamia wapi leo?" Naye Daudi alikuwa akisema, "Nchi ya kusini ya Yuda," au "nchi ya kusini ya Wayerameeli," au "nchi ya kusini ya Wakeni."
11Daudi hakumwacha hai mwanamume wala mwanamke ili kuwaleta Gathi, akiwaza, "Wasije wakatoa habari juu yetu, wakisema, 'Hivi ndivyo Daudi alivyofanya.'" Hii ndiyo iliyokuwa desturi yake muda wote alioishi katika nchi ya Wafilisti.
12Akishi akamwamini Daudi, akiwaza, "Amejifanya kuwa chukizo kubwa kwa watu wake Israeli; kwa hiyo atakuwa mtumishi wangu milele."