Sauli Ataka Kumuua Daudi
19 1Sauli akasema na Yonathani mwanawe na watumishi wake wote juu ya kumuua Daudi. Lakini Yonathani, mwana wa Sauli, alifurahia sana katika Daudi. 2Yonathani akamwambia Daudi, "Sauli baba yangu anataka kukuua, basi uwe mwangalifu asubuhi—kaa umejificha na usionekane. 3Nami nitatoka nikasimame kando ya baba yangu shambani ulipo, nami nitasema na baba yangu habari zako—kisha nitakuambia lolote nitakalogundua."
4Yonathani akanena mema juu ya Daudi kwa Sauli baba yake, akamwambia: "Mfalme asimtende dhambi mtumishi wake Daudi, kwa maana yeye hakukutenda dhambi wewe. Bali matendo yake yamekuwa mema sana kwako. 5Aliuhatarisha uhai wake ili kumpiga yule Mfilisti, na Baba yetu akaipatia Israeli yote ushindi mkuu. Wewe uliona ukafurahi. Kwa nini basi utende dhambi juu ya damu isiyo na hatia, kumuua Daudi bila sababu?"
6Sauli akamsikiliza Yonathani, akaapa, "Kama Baba yetu aishivyo, Daudi hatauawa."
7Yonathani akamwita Daudi, akamwambia mambo hayo yote, kisha akamleta kwa Sauli, naye Daudi akamtumikia kama kwanza.
8Vita vikatokea tena. Daudi akatoka, akapigana na Wafilisti, akawapiga kwa pigo kubwa, nao wakakimbia mbele yake.
9Lakini roho mbaya kutoka kwa Baba yetu ikaja juu ya Sauli alipokuwa ameketi nyumbani mwake, mkuki mkononi mwake, naye Daudi akapiga kinubi. 10Sauli akataka kumbandika Daudi ukutani kwa mkuki wake, lakini Daudi akajiepusha, na mkuki ukapiga ukutani. Daudi akakimbia, akapona usiku ule. 11Sauli akatuma watu kuilinda nyumba ya Daudi ili wamuue asubuhi. Mikali, mke wa Daudi, akamwonya: "Usipokimbia usiku huu, kesho utakuwa umekufa." 12Basi Mikali akamteremsha Daudi kupitia dirishani, naye akakimbia, akapona. 13Ndipo Mikali akaichukua sanamu ya nyumbani, akailaza kitandani, akaweka mto wa singa za mbuzi kichwani pake, akaifunika kwa nguo. 14Sauli alipotuma wajumbe kumkamata Daudi, Mikali akasema, "Yu mgonjwa."
15Basi Sauli akawarudisha wale wajumbe wamwone Daudi, akisema, "Mleteni kwangu katika kitanda, ili nimuue." 16Wajumbe walipoingia, tazama, sanamu ya nyumbani ilikuwa kitandani, na mto wa singa za mbuzi kichwani pake.
17Sauli akamwambia Mikali, "Mbona umenidanganya hivi, ukamwacha adui yangu apone?" Mikali akamwambia Sauli, "Yeye aliniambia, 'Niache niende, kwa nini nikuue?'"
18Daudi akakimbia, akapona, akaja kwa Samweli huko Rama, akamwambia yote Sauli aliyomtenda. Kisha yeye na Samweli wakaenda wakakaa Nayothi. 19Sauli akaambiwa, "Tazama, Daudi yuko Nayothi katika Rama." 20Sauli akatuma wajumbe kumkamata Daudi. Lakini walipoona kundi la manabii wakitoa unabii, na Samweli amesimama akiwa kiongozi wao, Roho wa Baba yetu ikawajia wale wajumbe wa Sauli, nao pia wakatoa unabii. 21Sauli akaambiwa; akatuma wajumbe wengine, nao pia wakatoa unabii. Sauli akatuma tena wajumbe mara ya tatu, nao pia wakatoa unabii. 22Mwishowe Sauli mwenyewe akaenda Rama, akafika kwenye kisima kikuu kilichoko Seku. Akauliza, "Wako wapi Samweli na Daudi?" Mtu mmoja akasema, "Wako Nayothi katika Rama."
23Akaenda huko Nayothi katika Rama, lakini Roho wa Baba yetu ikamjia yeye pia, naye akaenda akitoa unabii, hata alipofika Nayothi katika Rama. 24Yeye pia akavua mavazi yake, akatoa unabii mbele ya Samweli, akalala uchi mchana ule wote na usiku. Kwa hiyo watu husema, "Je, Sauli naye yuko miongoni mwa manabii?"