Ben-Hadadi Auzingira Samaria
20 1Ben-Hadadi mfalme wa Aramu akakusanya jeshi lake lote—wafalme thelathini na wawili pamoja naye, na farasi na magari ya vita. Akapanda, akaizingira Samaria, na kupigana nayo. 2Akatuma wajumbe ndani ya mji kwa Ahabu mfalme wa Israeli, akisema, "Ben-Hadadi asema hivi: 3'Fedha yako na dhahabu yako ni zangu, na wake zako walio bora na watoto wako ni wangu.'"
4Mfalme wa Israeli akajibu, "Kama usemavyo, bwana wangu mfalme: mimi ni wako, na vyote nilivyo navyo."
5Wajumbe wakarudi na kusema, "Ben-Hadadi asema hivi: 'Nilikutumia ujumbe nikidai fedha yako na dhahabu yako, wake zako na watoto wako. 6Lakini kesho karibu wakati huu nitatuma watumishi wangu wapekue jumba lako la kifalme na nyumba za watumishi wako, nao watatwaa na kuchukua kila kitu unachokithamini.'"
7Mfalme wa Israeli akawaita wazee wote wa nchi, akasema, "Angalieni vyema jinsi mtu huyu anavyotafuta shari. Alituma kudai wake zangu, watoto wangu, fedha yangu na dhahabu yangu, wala sikumkatalia."
8Wazee wote na watu wote wakamwambia, "Usimsikilize wala usikubali."
9Basi akawaambia wajumbe wa Ben-Hadadi, "Mwambieni bwana wangu mfalme, 'Yote uliyoyadai kwanza kwa mtumishi wako nitayafanya, lakini dai hili siwezi kulitimiza.'" Wajumbe wakaondoka na kupeleka jibu lake.
10Kisha Ben-Hadadi akatuma ujumbe: "Miungu na inipige vikali, kama mavumbi ya Samaria yatatosha kumpa kila mmoja wa wafuasi wangu konzi moja."
11Mfalme wa Israeli akajibu, "Mwambieni: 'Yeye ajifungaye silaha zake asijisifu kama yeye azivuaye.'"
12Ben-Hadadi na wafalme walipokuwa wakinywa katika mahema yao, akasikia haya akawaamuru watu wake, "Jipangeni," nao wakajipanga dhidi ya mji.
Baba Yetu Ampa Ahabu Ushindi
13Nabii mmoja akamjia Ahabu mfalme wa Israeli, akasema, "Baba yetu asema hivi: Je, unaliona jeshi hili kubwa? Leo nitalitia mkononi mwako, nawe utajua ya kuwa mimi ndimi Baba yako."
14"Kwa nani?" Ahabu akauliza. Nabii akajibu, "Baba yetu asema hivi: Kwa maofisa vijana wa wakuu wa majimbo." "Nani ataanzisha vita?" "Wewe," akasema.
15Basi Ahabu akawaita maofisa vijana wa wakuu wa majimbo—watu 232. Kisha akawaita waliosalia, Waisraeli wote—jumla 7,000. 16Wakatoka adhuhuri huku Ben-Hadadi na wafalme thelathini na wawili walioungana naye wakilewa katika mahema yao. 17Maofisa vijana wa wakuu wa majimbo wakatoka kwanza. Ben-Hadadi alikuwa ametuma wapelelezi, wakamwarifu, "Watu wanatoka Samaria."
18Akasema, "Ikiwa wametoka kwa amani, wakamateni hai; ikiwa wametoka kwa vita, wakamateni hai."
19Maofisa vijana wa wakuu wa majimbo wakatoka nje ya mji na jeshi likiwafuata nyuma. 20Kila mtu akamuua adui yake. Waaramu wakakimbia, Israeli akiwafuatia, lakini Ben-Hadadi mfalme wa Aramu akaponyoka juu ya farasi pamoja na wapanda farasi kadhaa. 21Mfalme wa Israeli akasonga mbele na kuwashinda farasi na magari ya vita, akiwasababishia Waaramu hasara kubwa. 22Baadaye nabii akamjia mfalme wa Israeli: "Jiimarishe na ufikiri kwa makini juu ya yale unayopaswa kufanya, kwa sababu majira ya machipuko yajayo mfalme wa Aramu atakushambulia tena."
23Wakati huohuo maofisa wa mfalme wa Aramu wakamwambia: "Miungu yao ni miungu ya milimani; ndiyo maana walitushinda. Tupigane nao katika nchi tambarare, nasi hakika tutawashinda. 24Fanya hivi: waondoe wafalme wote katika nafasi zao za amri, na uweke maofisa wengine mahali pao. 25Kusanya jeshi kama lile ulilolipoteza—farasi kwa farasi, gari kwa gari—kisha upigane na Israeli katika uwanda. Ndipo hakika tutakuwa na nguvu zaidi." Akawasikiliza akafanya hivyo.
26Majira ya machipuko yaliyofuata Ben-Hadadi akawakusanya Waaramu, akapanda Afeki kupigana na Israeli. 27Wana wa Israeli walipokusanywa na kupatiwa mahitaji, wakatoka kuwakabili. Israeli wakapiga kambi wakiwakabili kama makundi mawili madogo ya mbuzi, huku Waaramu wakiijaza nchi.
28Mtu wa Mungu akamjia mfalme wa Israeli, akasema, "Baba yetu asema hivi: Kwa sababu Waaramu wanadhani BWANA ni mungu wa vilima, si wa mabonde, nitalitia jeshi hili lote kubwa mkononi mwako, nawe utajua ya kuwa mimi ndimi Baba yako."
29Kwa siku saba walipiga kambi wakikabiliana; siku ya saba vita vikaanza. Katika siku moja wana wa Israeli wakawaua askari wa miguu wa Waaramu 100,000. 30Waliosalia wakakimbilia Afeki, mahali ukuta ulipowaangukia watu 27,000 kati yao. Ben-Hadadi akakimbilia mjini na kujificha katika chumba cha ndani.
31Watumishi wake wakasema, "Tumesikia ya kwamba wafalme wa nyumba ya kifalme ya Israeli ni wenye huruma. Twendeni kwa mfalme wa Israeli tukiwa na nguo za matanga viunoni mwetu na kamba vichwani mwetu; huenda atayaacha maisha yako."
32Basi wakiwa na magunia viunoni mwao na kamba vichwani mwao, wakamjia mfalme wa Israeli, wakamsihi, "Mtumishi wako Ben-Hadadi asema, 'Tafadhali niache niishi.'" Akajibu, "Je, angali hai? Yeye ni ndugu yangu."
33Watu wale wakalichukua kama ishara njema, wakayashika maneno yake kwa haraka. "Naam, ndugu yako Ben-Hadadi!" wakasema. "Nendeni, mleteni," akasema mfalme. Basi Ben-Hadadi akatoka, naye Ahabu akampandisha katika gari lake la vita.
34"Nitakurudishia miji ambayo baba yangu aliuchukua kutoka kwa baba yako," Ben-Hadadi akasema, "nawe waweza kujiwekea maeneo yako ya biashara katika Dameski, kama baba yangu alivyofanya katika Samaria." Ahabu akasema, "Kwa masharti haya nitakuachia huru." Basi akafanya agano naye na kumwacha aende zake.
Nabii Amkabili Mfalme
35Kwa neno la Baba yetu mmoja wa wana wa manabii akamwambia mwenzake, "Tafadhali nipige." Lakini mtu yule akakataa kumpiga.
36Nabii akasema, "Kwa sababu hukuitii sauti ya Baba yetu, mara utakapoondoka kwangu simba atakuua." Mtu yule alipoondoka, simba akamkuta na kumuua.
37Nabii akampata mtu mwingine, akasema, "Tafadhali nipige." Basi mtu yule akampiga na kumjeruhi.
38Kisha nabii akasimama kando ya njia akimngojea mfalme, akijibadilisha kwa kitambaa cha kufunga machoni pake. 39Mfalme alipopita, nabii akalia kwa sauti, "Mtumishi wako aliingia katikati ya vita, na mtu mmoja akageuka, akaniletea mateka, akasema, 'Mlinde mtu huyu. Akipotea, uhai wako utakuwa badala ya wake, ama utalipa ratili sabini na tano za fedha.' 40Wakati mtumishi wako alipokuwa akijishughulisha huku na huku, mtu yule akatoweka." Mfalme wa Israeli akasema, "Hiyo ndiyo hukumu yako; wewe mwenyewe umeiamua."
41Nabii akakiondoa kwa haraka kitambaa machoni pake, na mfalme wa Israeli akamtambua kuwa ni mmoja wa manabii.
42Akamwambia mfalme, "Baba yetu asema hivi: Kwa sababu ulimwacha aende zake yule mtu niliyemhukumu maangamizi, itakuwa uhai wako badala ya uhai wake, watu wako badala ya watu wake."
43Akiwa na huzuni na hasira, mfalme wa Israeli akaenda nyumbani, akarudi Samaria.